13/10/2023
KUELEKEA MAADHIMISHO YA MIAKA 50, NECTA YAZINDUA ZOEZI LA UPANDAJI MITI MUFINDI
Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA) linatarajia kutimiza miaka 50 tangu kuanzishwa kwake ifikapo mwezi Novemba mwaka huu. Ikiwa sehemu ya shughuli mbalimbali zitakazofanywa kuelekea kilele cha maadhimisho hayo, Baraza linakusudia kupanda miti zaidi ya 100,700 nchi nzima katika shule za Msingi na Sekondari pamoja na Vyuo vya Ualimu ifikapo Disemba, mwaka huu.
Taarifa hiyo ilitolewa na Katibu Mtendaji wa NECTA, Dkt. Said Ally Mohamed wakati akizungumza na walimu na wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Mufindi, Mkoani Iringa wakati akizindua zoezi la upandaji miti lililoshirikisha Shule ya Msingi ya Mtili βAβ ambapo zaidi ya miti 3,200 ilipandwa.
Dkt. Mohamed alisema NECTA ni moja ya Taasisi ambayo ni mtumiaji mkubwa wa karatasi kwa ajili ya uendeshaji wa mitihani mbalimbali katika ngazi ya elimu Msingi, Sekondari na Vyuo vya Ualimu.
βKwa miaka mitano iliyopita, kuanzia mwaka 2018 hadi 2023, zaidi ya watahiniwa milioni 24 walisajiliwa kufanya mitihani mbalimbali. Watahiniwa hawa k**a ni Darasa la Saba, mmoja anafanya mtihani kwa masomo sita na kila mtihani unakuwa na karatasi ngapi, karatasi za majibu ngapi, ukijumuisha utaona tuna mahitaji makubwa ya karatasi,β alisema Dkt. Mohamed.
Pia, Katibu Mtendaji huyo alibainisha kuwa kila sensa ya watu inapofanyika nchini huonyesha kuwepo kwa ongezeko la watu. Kwa mfano, wakati sensa ya mwaka 2002 tulikuwa milioni 34.4, idadi ya watanzania iliongezeka na kufikia milioni 44.9 mwaka 2012. Aidha, sensa ilipofanyika mwaka jana idadi ya watu imeongezeka kufikia milioni 61.7. Katibu aliongeza kuwa idadi ya watu ikiongezeka maana yake kuna ongezeko la watahiniwa hivyo lazima Baraza lifikirie mipango ya maendeleo ya kiteknolojia ili kuboresha huduma kulingana na ongezeko la watahiniwa.
Katibu huyo aliongeza kuwa takwimu kidunia zinaonesha kuwa matumizi ya karatasi kwa miaka 40 iliyopita yameongezaka kwa zaidi ya asilimia 400. Ni muhimu kasi ya upandaji miti ikaongezwa kwani wakati miti bilioni 15 inakatwa kila mwaka kwa matumizi mbalimbali duniani, ni miti bilioni 1.9 tu ndiyo inayopandwa kwa mwaka.
βBaraza la Mitihani tukaona kupitia maadhimisho ya miaka 50, tuwaombe wadau katika vituo vyetu vya mitihani, katika shule za msingi, sekondari na Vyuo vya Ualimu wapande miti kwani k**a kila shule ikishiriki kupanda miti, tukaisimamia ukuaji wake tutakuwa tumefanya kitu kikubwa kwa nchi yetu na ulimwengu kwa ujumla,β alisema Dkt. Mohamed.
Katika hotuba yake, Dkt. Mohamed alishukuru Wakala wa Huduma za Misitu nchini (TFS) kwa kuwa tayari kutoa miche ya miti katika shule mbalimbali nchini katika kipindi cha mwezi Oktoba hadi Disemba mwaka huu.
Aidha, Baraza limepanga kufanya Kongamano la Kitaaluma litakalofanyika Novemba 29 mwaka huu, Zanzibar, kuandika Kitabu cha Historia ya Baraza la Mitihani na kufanya maonesho katika viwanja vya Mn**i Mmoja kuanzia Novemba 30 hadi Disemba 3, mwaka huu kabla ya sherehe za kilele cha maadhimisho hayo zitakazofanyika katika ofisi za Baraza mnamo Desemba 4, mwaka huu.