08/03/2024
WOMEN’S DAY: PONGEZI NA TAFAKURI
Leo tumekumbuka na kuadhimisha siku ya wanawake duniani. Tumetuma salaam na kusema maneno mazuri juu yao. Tumepost picha za mama zetu, wake zetu, shangazi zetu, dada zetu, mabinti zetu na marafiki zetu wa k**e waliotoa mchango mkubwa katika maisha yetu.Hakika akina mama ni nguzo yetu muhimu. Ninajiliuliza, hivi mimi ningekuwaje pasipo akina mama hawa?
Tunapoendelea kuwapongeza na kuadhimisha siku hii muhimu kwa mwaka huu, ninapenda kwa leo kuzungumzia wanawake wanaoishi vijijini.
1. Kwa wanaotoka katika mazingira ya vijijini k**a mimi, mtakubaliana na mimi kwamba wanawake au akina mama wanafanya kazi nyingi sana, kuanzia asubuhi hadi usiku. Katika familia zilizo nyingi, kwa kawaida, akina mama ndio huamka wakiwa wa kwanza na ndio huenda kulala wakiwa wa mwisho.
2. Katika familia nyingi, ni akina mama wanaodamka asubuhi sana kwenda mtoni kuchota maji. Wakirudi nyumbani huandaa kifungua kinywa kwa ajili ya familia (k**a kipo cha kuandaa). Wakati huo huo, akina mama huwaandaa watoto ili wawe tayari kwenda shuleni. Hawaishii hapo, bali pia huwandaa waume zao ili waende kazini kwao. Siku huendelea hivyo hadi usiku. Mama huenda kulala anapohakikisha wote wamekwenda kitandani. Wengi wakifika kitandani napo hukutana na majukumu mengine mazito ya yanayowasubiri kufanya, majukumu yasiyojali uchovu walioupata mchana kutwa! Hubeba/hubebeshwa mimba wakati mwingine pasipo ridhaa yao. Hulea mimba/mtoto tumboni. Maisha ya akina mama wengine huwa hatarini wakati wa kujifungua. Wengine tumewahi kuguswa na hilo!
Wakibahatika kujifungua salama, huingia mwenye shughuli nzito ya malezi ya watoto. Wanafanya kazi hiyo ya kulea hadi watoto wao wanapokuwa majitu mazima ya zaidi miaka hamsini k**a mimi. Ukimtembelea mama, yeye huangaika sana kukutafutia kitu cha kwenda nacho k**a vile maharage, mahindi, ndizi, nk. Kwa sababu ya upendo alionao, yuko tayari kutoa hata kile alichobakiza nyumbani kwake. Wanaotoka Dar es Salaam, wakifika vijijini, hao hubeba madebe au magunia k**a zawadi.
Kuwa mama na mkulima mdogo ni shughuli, ni shughuli, ni shughuli!
3. Ninatoka katika mazingira ya vijijini ambapo watu au familia nyingi hutegemea shughuli za kilimo. Wengi wao ni wakulima wadogo wadogo. Kwa mtu ambaye hajawahi kujihusisha na shughuli za kilimo k**a mkulima mdogo, hawezi kuelewa nini ninachokimaanisha.
Ukweli ni kwamba wakulima wadogo (wengi wao wakiwa ni wanawake) wanaishi maisha magumu sana. Katika maadhimisho ya siku ya wanawake k**a leo, ninatamani kila mmoja, apate nafasi ya kutafakari namna ya kupunguza taabu wanazokumbana nazo mama zetu, shangazi zetu, dada zetu na mabinti zetu wanaoishi vijijini.
Hilo lingekuwa jambo jema, badala ya kuwaandamanisha na kwakusanya ili wacheze ngoma na kuambiwa maneno matamu matamu bila kutatatua shida walizonazo.
4. Kimsingi, wakulima wadogo wadogo ndio wazalishaji wakubwa wa chakula duniani. Hata hivyo, wao wenyewe mara nyingi hukosa chakula cha kutosheleza familia zao. Hadi chakula kizalishwe na kuwafikia walaji sokoni, akina mama na watu wote wanaojishughulisha na kazi za kilimo (k**a wakulima wadogo) humenyeka sana. Kwa wanaonunua chakula gulioni au kwenye supamaketi (k**a huku Ulaya), wanachokijua ni eneo au shelfu zenye vyakula vilipopangwa. Wanajua shelf ya viazi iko wapi, nyanya ziko wapi, vitunguu viko wapi, matunda yako wapi, nk. They just pick and go. Hawana muda wa kujishughulisha na kadhia na taabu nyingi wanazopata wakulima wadogo wadogo wakati wa kuzalisha chakula hicho.
5. Wakulima wadogo wadogo hulima kwa jembe la mkono. Kutumia jembe la mkono kunachosha sana na kuchakaza miili ya akina mama! Kutumia jembe la mkono siyo kufanya mazoezi k**a mtu mmoja alivyoniambia hivi karibuni baada ya kuwasilisha mada kuhusu hali ya wakulima wadogo wadogo mahali fulani. Kilimo cha jembe la mkono kinachakaza kweli kweli. Ili mtu amalize kulima ekari moja, anahitaji takribani mwezi mmoja, kitu ambacho trekta hufanya kwa pungufu ya masaa mawili.
6. Baada ya kuandaa shamba, wakulima na hasa wanawake hupanda mazao k**a vile maharage, mahindi na nafaka zingine kwa kutumia zana duni za mkono k**a vile “akahosho” au “akachumu” (wanaojua kanaitwaje kwa Kiswahili watanisaidia). Ili amalize kupanda maharage kwenye ekari hiyo moja, anahitaji wiki moja au mbili za kujipinda mgongo. Mara nyingi, ni akina mama au dada zetu ambao hufanya shughuli hizo, wakati mwingine wakiwa wamebeba watoto migongoni mwao. Kisha hujipinda migongo kufanya palizi kwa mikono yao. Ukiangalia vidole na miganja vya wakulima wadogo utashangaa. Vina makovu kila mahali. Visigino vya miguu yao vimejaa "enkwakara" (sijui zinahitwaje kwa Kiswahili). Kwa Kiingereza, sidhani kuna neno la kumaanisha neno "enkwakara" (michirizi kwenye visigino vya miguu) kwani hawazijui.
Shughuli za kilimo cha wakulima wadogo hutegemea mvua kwa asilimia mia moja. Kukosekana kwa mvua kunamaanisha kukosekana kwa mavuno na njaa kwa familia. Kukosekana kwa mvua kunamaanisha kukosekana kwa mahitaji mengine muhimu katika familia. Kukosekana kwa mvua kunamaanisha kukosekana kwa mahitaji ya shule kwa watoto, nk. Ni maisha magumu na ya kubahatisha!
Ndiyo maana nawaelewa vijana wengi wanaoamua kukimbia vijiji na kukimbilia mijini ambako hudhani kuna maisha bora na mepesi. Nako huko hukosa kazi au hufanya kazi za umachinga. Wanatafuta kazi bora kuliko kuwa mkulima mdogo mdogo, anayetaabika siku kwa siku hadi anapoitwa mbinguni kwa Muumba wake.
6. Kuwa mkulima mdogo ni jambo gumu sana. Mara nyingi, mavuno yanayopatikana hayalingani kabisa na nguvu na muda wanaoutumia wakulima kufanya kazi hizo nzito za uzalishaji. Sidhani k**a kuna mkulima mdogo ambaye huhesabu muda na nguvu anazozitumia katika kuzalisha. Hata angefanya hivyo, hana chaguo lingine zaidi ya kuendelea kupambana na hali yake huko huko kijijini. Hakuna mtu anayependa hali k**a hiyo. Lakini watu wanalazimika kuishi maisha ya jinsi hiyo na katika hali ya umaskini uliokithiri. Ni aibu kwa jumuiya ya kimataifa kwa kushindwa kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu, lengo mojawapo likiwa ni kutokomeza umaskini duniani kote ifikapo 2030. Malengo hayo yamebaki tu vinywani mwa watu. Yanatajwa wakati wa warsha na makongamano ya kitaifa na kimataifa, lakini sioni jitihada za makusudi za kutokomeza umaskini duniani, ambao unatesa watu wengi hasa wakulima wadogo wadogo.
7. Kinachoumiza zaidi ni kwamba, baada ya wakulima hao wadogo wadogo kuvuna mazao yao na kuyapeleka sokoni (mara nyingi kichwani na kwa kutembea umbali mrefu), wakulima huambulia kupata kipato kidogo sana (namaanisha kidogo sana) ambacho pia huamuliwa na wachuuzi sokoni. Maskini, wakulima hawapangi bei za mazao yao.
Kutokana na hali hiyo, maisha ya wakulima wadogo wadogo yanaendelea kuwa duni siku kwa siku, kwani wananyonywa na kudhulumiwa kila upande na katika kila hatua miaka nenda rudi. Siyo tu kwamba jasho lao linanyonywa na wachuuzi, bali pia na mifumo iliyopo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa nchini na duniani kwa ujumla. Tuna mifumo ya kinyonyaji sana nchini na duniani. Mifumo inayoendelea kuwafanya wachache kuendelea kutajirika hali walio wengi na hasa akina mama wakiendelea kutaabika na kuwa duni. Wakienda sokoni kuuza mazao yao, nako huko hukutana na mtoza ushuru mkali ambaye anachokijua tu ni kukusanya mapato aliyoambiwa au kujipangia kumshirikisha mzalishaji. Wakusanyaji wa ushuru wengine huweka pesa wanazokusanya mifukoni mwao.
8. Katika mazingira k**a yaliyoko nchini Tanzania kwa sasa ambapo bei ya bidhaa za madukani naza viwandani zimepanda sana (kuliko maelezo), ni wakulima wadogo wadogo, wamachinga na wabangaizaji wanaoteseka zaidi. Hivi kwa mfano, ni mkulima mdogo gani anayeweza kununua kilo ya sukari kwa bei ya zaidi ya shilingi 4,000/= za Kitanzania. Kimsingi, bei hiyo ni kubwa zaidi ya bei ya sukari nchini Ujerumani licha ya kipato cha Mjerumani na Mtanzania kutofautiana sana k**a ilivyo mashariki na magharibi! Hivi mkulima wa nanasi, kwa mfano, anahitaji kuuza nanasi ngapi ili anunue kilo moja ya sukari?
Nilipokuwa Karagwe hivi karibuni, niliwahoji wakulima wachache ambao walisema wanahitaji kuuza nanasi tano hadi sita ili kununua kilo moja ya sukari. Kwa wanaouza ndizi, wakati mwingine mkungu mmoja wa ndizi (inayotoka kwa mkulima mdogo), inauzwa kwa shilingi 4,000/=, sawa na bei ya kilo moja ya sukari.
9. Mfumuko wa bei ulioko nchini Tanzania unatisha sana. Narudia tena: "mfumuko wa bei Tanzania unatisha sana" na ninahisi viongozi wetu wa nchi hawajatilia maanani sana jambo hili. Inawezekana ni kwa sababu yenyewe hawaguswi moja kwa moja na mfumuko huo.
Mfumuko mkubwa wa bei za bidhaa nyingi umefanya maisha kuwa magumu sana. Umewafanya watu waone mahitaji mengine yaliyo muhimu (k**a vile sukari ) kuwa ni anasa. Bei za bidhaa nyingi hazishikiki! Kwa mtu ambaye hajawahi kuishi kijijini au kuishi maisha ya kubangaiza mitaani, hawezi kuelewa hata kelele zipigwe kiasi gani!
Wanasiasa wengi hujifanya kusikia kelele za wakulima wadogo wadogo, wamachinga, wabangaizaji mitaani nk., pale tu wanaposaka kura za makundi hayo.
Jamani wakulima wadogo wadogo wana taabu sana! Ninatamani katika maadhimisho haya akina mama na sisi sote tufikishe kelele na kilio hiki kwa Mama yetu namba moja na msikivu, Mama Samia! Wanaompenda, tumwambie ukweli mweupe kwamba hali ya maisha katika nchi yetu inatisha. Bei ya mafuta inatisha. Kodi kwa wafanya biashara zinatisha. Biashara mbalimbali nyingi ziko mbioni kufa kutokana na kodi na matozo yanayoongozeka siku hata siku. Mwathirika namba moja ni mkulima mdogo anayeishi kijijini.
10. Jambo la pili la kukumbuka na kutafakari katika maadhimisho haya ya siku ya wanawake duniani kwa mwaka huu, ni suala la maji.
Vijijini hakuna maji ya bomba! Pamoja na shughuli nzito za shambani, wakulima wadogo hulazimika kutembea kilometa kadhaa kwenda mtoni (chanzo cha maji) kutafuta maji. Mtu akiwa na maji ya bomba nyumbani kwake anaonekana k**a tajiri. Kuwa na maji ya bomba (tena ya mgao) ni kipimo cha utajiri Tanzania. Ni anasa! Mtu mmoja aliwahi kusema: “hivi ni vitu vya wachache!” Sijui k**a kuna mtu amewahi kufanya utafiti kujua ni watu wangapi wako kwenye kundi la matajiri kwa sababu ya kuwa na maji majumbani mwao. "Hivi ni vitu vya wachache!"
Ni jambo linalotafakarisha sana kwa mtu anayetaka kutafakari!
11. Agenda ya maji inatumiwa sana na wanasiasa wakati wa chaguzi. Utasikia wengi wakisema, “mkinichagua mimi, nitahakikisha kwamba ninawatua akina mama wote ndoo za maji vichwani!” Na wengi wetu huwa tunawashangilia sana na kuwapigia makofi mengi wanasiasa wanaotoa ahadi za "kumtua mama ndoo kichwani".
Tangu mimi nilipoanza kupiga kura mwaka 1990 nikiwa na umri wa miaka 21 hadi leo, nimeendelea kusikia agenda au sera hii ya kumtua mama ndoo kichwani. Sijui, ngoja tusubiri tuone k**a sera hiyo itajitokeza katika uchaguzi unaofuata hivi karibuni!
12. Wapo akina mama wengi waliosubiri "kutuliwa ndoo kichwani" hadi wakafariki dunia wakiwa bado na ndoo kichwani mwao! Wangefufuka leo, wangeshangaa kukuta watu bado wakiomba kura kwa kutaja habari ya kuwatua akina mama ndoo kichwani. Ninatamani asiwepo mwanamke yeyote (ambaye ameshuhudia maadhimisho ya siku yao mwaka huu) wa kufariki akiwa bado amejitwika ndoo kichwani mwake. Mahali pengine, huwezi kusikia mtu akitaja suala la maji k**a agenda ya kisiasa kwani maji ni hitaji la kwanza na la msingi la binadamu. Ni haki ya binadamu ya msingi sana! Kwa wanaopambana kuttetea haki za binadamu (wengine kutoka Ulaya na Marekani), hebu anzeni na tatizo hilo la maji, baa la njaa, umaskini, huduma duni za kiafya na mengine katika nchini Tanzania na kwingineko duniani hasa barani Afrika.
13. Tafakari hii imenikumbusha jambo!
Siku tulipo-drill na kupata maji shuleni kwetu, watu wote tuliokuwepo tulishangilia sana na hata ku-celebrate! Furaha na mashangilio tuliyokuwanayo siku ile yalinifanya nitafakari na kutoa comment ambayo napenda kufunga nayo mada yangu hii ndefu: “Ni jambo la ajabu na la kushangaza kwamba bado nchini mwetu, tunashangilia na ku-celebrate tunapopata hitaji la msingi kabisa k**a maji, jambo ambalo siyo hoja katika nchi zilizoendelea!”
Jambo ambalo nimeona wenzetu (kwa mfano kutoka Ulaya) wakilifurahia na hata kulishangilia ni pale wanapokuta au kuona "swimming pool" mahali ambapo hawakutarajia! Lakini kushangilia na ku-celebrate kwa sababu ya kupata maji ya matumizi ya kawaida, hilo ni letu Afrika na tunabidi tuwe na hasira sana kuondoa hali hiyo.
Still a long way to go?
Happy women's day!