13/12/2019
JE SAMAKI HUNYWA MAJI?
Nauliza nijibiwe,mwenzenu nione raha
Langu jibu nipatiwe,nasaka yenu nasaha
Kwa swali msikerewe,naapa sina mzaha
Nauliza nijibiwe, je samaki hunywa maji?
Nauliza nijibiwe,je samaki hunywa maji
Pia nami nitambuwe,nijivishe langu taji
La ukweli nilijuwe,niwapiku wajuaji
Nauliza nijibiwe,msafiri nije jua
Nauliza nijibiwe,msafiri nije jua
Samaki niwaelewe,nipate kuwatambua
Midomo siwapanuwe,kwa kijiko kuwapea
Nauliza nijibiwe,maji huyanywea vipi?
Nauliza nijibiwe,maji huyanywea vipi?
Moyo wangu unituwe,nijue taaza wapi
Nimewafuga mwenyewe,sijui nifanye lipi
Nauliza nijibiwe,si ujinga kuuliza
Nauliza nijibiwe,si ujinga kuuliza
Naona bora wapewe,wasitete kawabeza
Makini nish*takiwe,zao haki kapuuza
Nauliza nijibiwe,mwenye jibu alitoe
Nauliza nijibiwe,mwenye jibu alitoe
Kesho nisisingiziwe,kama kosa nikosoe
Narai haki wapewe,na maji niwapatie
Nauliza nijibiwe,Msafiri nifahamu
Nauliza nijibiwe,Msafiri nifahamu
Kwa bayana niambiwe,kujua ninayo hamu
Kinishe na kiwewe,nitulie kiwa humu
Nauliza nijibiwe, Je samaki hunywa maji?
Msafiri Makini
Mugendi Mutegi